Sunday, September 9, 2012

KUTOKA TANZANIA DAIMA

Mwangosi aliuawa hivi
•  SIMULIZI YA SHAHIDI

na Mwandishi wetu

SEPTEMBA 2, 2012, polisi waliua kikatili mwandishi wa habari wa kituo cha Channel Ten, Daudi Mwangosi, katika Kijiji cha Nyololo, mkoani Iringa. Alikufa mbele ya Kamanda wa Polisi mkoani humo, Michael Kamuhanda, wakati polisi hao walipovamia ofisi ya Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA) ili kuwatawanya wasifungue tawi la chama chao katika kijiji hicho.

Mmoja wa watu walioshuhudia tukio zima, ni mwandishi wa Tanzania Daima, Abdallah Khamis. Ifuatayo ni simulizi ya kile alichokiona wakati polisi wanaondoa uhai wa Mwangosi.

SIKU hiyo asubuhi tulipata taarifa kuwa Kamanda wa Polisi mkoani humo (RPC), Michael Kamuhanda, alipanga kukutana na waandishi wa habari majira ya saa 2.30 ambapo waandishi walifika akiwemo Daudi Mwangosi.
Tukiwa katika chumba cha mikutano katika jengo la polisi Mkoa wa Iringa, Kamanda wa mkoa huo, alifika akiongozana na maafisa wake wawili na kuanza kutusomea taarifa ya zuio la mikutano ya CHADEMA iliyokuwa iendelee siku hiyo baada ya kupisha zoezi la awali la sensa.

Alitusomea zuio hilo na kutuambia hata viongozi wa CHADEMA wameshataarifiwa usiku wa Septemba Mosi. Tukamuuliza mbona taarifa za sensa zinaeleza kuwa kuna mafanikio kwa asilimia 95 na waliobaki wanatakiwa waende kwa viongozi wao? Akatujibu kuwa hilo ni agizo na linapaswa litekelezwe na CHADEMA.

Waandishi hawakuchoka kumuuliza maswali RPC na moja ya maswali yaliyoonekana kumkera kamanda huyo ni lile lililotoka kwa Daudi Mwangosi kuwa mbona wakati wa mwanzo walipozuia mikutano ya CHADEMA mkoani humo mikutano mingine ya CCM ndani ya mkoa huo na sehemu nyingine nchini ilikuwa inaendelea.

Swali lingine la Mwangosi lilimtaka kamanda huyo kutumia busara katika hali iliyopo kwa lengo la kuepusha maafa yanayoweza kutokea endapo angeendelea kushikilia msimamo wake kuwa hakuna mkutano wa aina yoyote utakaofanyika.

Baada ya maswali hayo, tulimuona Kamanda Kamhanda akiwa amekunja sura kama ishara ya kuchukizwa na maswali ya Mwangosi ambaye aliongeza swali lingine kwamba, “inaonekana Kamanda umechukia kutoka ndani ya moyo wako” na kamanda akajibu “ni lazima nichukie na nawachukia hawa CHADEMA kwa kuwa ninaipenda kazi yangu na pia ninakaribia kustaafu na sitaki kustaafu vibaya.”

Baada ya hapo maafisa waliokuwa na RPC waliandika ujumbe kwenye karatasi na wakamfikishia mkuu wao, na baada ya muda mkutano huo ulimalizika huku kukiwa na kauli za utani wa hapa na pale kati ya waandishi wa habari na baadhi ya askari juu ya kwenda kuripoti matukio ya siku hiyo.
Tulipokuwa nje ya jengo, Mwangosi, kwa kuwa ni mwenyeji wa mkoa huo, alikuwa akitaniana na mmoja wa askari aliyevaa kiraia, ambaye alimwambia kuwa, “huko hakutakuwa na kujuana na kuna uwezekano wa watu kufa.”
Mwangosi alijibu papo hapo kuwa hilo haliogopi kwa kuwa kifo ni ada ya mja yeyote na kwamba ataogopa kama mtu atamuahidi kuishi milele.
Baada ya hapo, kila mmoja alitawanyika katika eneo lake, na majira ya saa saba mchana baadhi ya waandishi walikutana ili kuanza safari katika Wilaya ya Mufindi kwa ajili ya kuripoti mkutano wa ndani wa CHADEMA na ufunguzi wa matawi.

Waandishi wa habari hao pamoja na mimi ni Godfrey Mushi (Nipashe), Olver Motto (Star Tv), Renatus Mutabuzi (ITV), Clement Sanga (Mwananchi), Joseph Senga (Tanzania Daima) na Tumaini Makene (Ofisa Habari wa CHADEMA).

Tulipofika katika mji wa Mafinga, tulipata chakula cha mchana kabla ya kwenda katika Kijiji cha Nyololo, na muda wote huo Mwangosi alikuwa hajaungana nasi.

Tuliondoka Mafinga kuelekea Nyololo huku mwenzetu Clement Sanga akiwasiliana na Mwangosi aliyesema yuko katika basi na angeungana nasi tukiwa Nyololo. Tulipofika pale tuliona askari wachache wakiwa wamesimama barabarani huku gari lao moja likiwa linajaza mafuta katika kituo cha mafuta kilichopo eneo hilo.

Tukiwa njia ya kwenda Mbeya, mita kama 100 kutoka katika mji wa Nyololo, kushoto kwetu tuliziona ofisi za CHADEMA zikiwa zimepambwa kwa bendera nyingi, na kulia kwake tuliona magari manne ya askari waliokuwa na silaha.

Baada ya kupita eneo hilo, gari moja la polisi lilikuwa likitufuata, na hapo tulishauriana kugeuza gari kurudi katika eneo la mji. Tulipofanya hivyo, na gari la polisi lilisimama.

Wakati tunarudi katika eneo la mji, tuliegesha gari pembeni. Baadhi ya waandishi wa habari waliingia mitaani kwa makubaliano kuwa baada ya dakika 10 tuwe tumerejea kwa ajili shughuli iliyotuleta - kushuhudia ufunguzi wa tawi hilo jipya la CHADEMA.

Muda huo ulipofika, tulirejea, lakini Mwangosi alikuwa hajaungana nasi.
Baadaye tulianza kuona baadhi ya magari yakiwa na bendera ya CHADEMA yakipita moja baada ya jingine.

Kuwasili kwa Mwangosi eneo la Nyololo
Saa 10.22 Mwangosi aliwasili kwa basi ambalo sikumbuki kama ni Hood au Abood; na muda huo huo tukawaona askari wakiyatoa magari yao kutoka mafichoni na kuingia upande wa kulia wa mji wa Nyololo kwenye ofisi za kata za CHADEMA.

Wakati askari wakiwa wanapita walikuwa wakisema Dk. Slaa anatokea eneo la Wami. Waandishi wa habari wakawa wamejiandaa kwenda kwa kufuata njia hiyo.

Tuliegesha gari letu mbali. Mwangosi ambaye hakuwepo awali, akataka kuchukua pikipiki ili awahi. Kwa kuwa muda huo nilikuwa naye, nikamsihi kuwa hana haja ya kuingia gharama kwa kuwa gari la waandishi wa habari lipo. Akanielewa, na tukaingia katika gari hilo, huku akiwa amempakata Oliver Motto wa Star Tv.

Tulipoenda kama mita 50 hivi, tulikutana na msafara wa CHADEMA ukiwa unaelekea tunakotoka. Gari la waandishi wa habari na magari ya polisi yakalazimika kukaa pembeni kuyapisha, kisha wakaungana nao kuelekea katika ofisi za tawi za chama hicho.

Ofisi za tawi za CHADEMA katika mji huo wa Nyololo zipo mita zaidi ya 100 upande wa kushoto wa bararara ya kuelekea Mbeya. Awali polisi walikuwa wameegesha magari yao barabarani wakati CHADEMA wakielekea katika ofisi zao.

Hakukuwa na vurugu yoyote. Ghafla kiongozi wa polisi ambaye alikuwepo pale - tulimtambua kwa jina la Mnunka - aliwaamuru askari wake watoe ilani kwa kunyoosha bendera kubwa nyekundu juu na kuwataka CHADEMA waondoke katika ofisi zao. Tukapiga picha tukio hilo.

Wakati askari wakijiandaa kuwafuata wana CHADEMA katika ofisi zao, alitokea mtu aliyevaa shuka na kujifunga kitambaa kichwani ambaye baadaye alijitambulisha kama mkuu wa upelezi mkoa (RCO), akawaamuru wenzake waende katika ‘target’ lakini wasithubutu kutumia nguvu bila amri.

Hapa ndipo tulipoanza kupata wasiwasi ni nani anatoa amri kwa kuwa yule wa mwanzo, Mnunka alijiapiza kuwa wamechoka kuvumilia, na kwamba siku hiyo CHADEMA watawatambua. Hata tulipomuuliza maana ya kauli ile, hakutupa jibu la kueleweka.

Katika hali hiyo, mtu aliyejitambulisha kama ndie RCO alizungumza na viongozi wa CHADEMA, wao wakamwambia wako katika kikao cha ndani. Yeye akasema jukumu lake ni kuhakikisha usalama unakuwepo, na kwamba kama ni suala la kikao cha ndani hawawezi kuzuia.

Tulitaka kupata ufafanuzi wa masuala mbalimbali kutoka kwa RCO ambaye alikuwa akizungumza kwa simu na mtu ambaye baadaye ilikuja kubainika kuwa ni Kamanda wa Polisi wa Mkoa (RPC), akawa anamueleza kuwa hali ni salama. Alituahidi waandishi wa habari tuvute subira “kwa kuwa mwenye
mkoa amewasili.”

Baada ya kuwasili kwa RPC Kamuhanda, Kamanda wa FFU, Mnunka alienda akamnong’oneza jambo. Pale pale, Kamuhanda akaonekana kukasirika. Akaagiza CHADEMA wasimamishe shughuli yao mara moja.

Tulitaka kujua tafsiri ya mkutano wa ndani kwa Jeshi la Polisi ni ipi, ni kwa wahusika kukaa ndani au ni ule mkutano utakaowahusisha wanachama peke yao kama ambavyo CHADEMA walikuwa wanasema pale. RPC akatujibu kuwa hilo halielewi na yeye si mwanasiasa.

Baada ya maelezo hayo, waandishi wa habari tulimbana RPC kwa maswali hata ikafikia hatua ya kamanda huyo kuanza kuwanyooshea vidole baadhi yetu, huku alimlalamikia Mwangosi kwamba kwanini hakushiba na majibu aliyopewa tangu asubuhi.

RPC akaniambia mimi kwamba nauliza maswali yanayopingana na mtazamo wa jeshi hilo; akamwambia Mutabuzi kuwa anamfahamu.

Baada ya hali hiyo, CHADEMA walimaliza mkutano wao katika ofisi za tawi na wakawa wanaelekea katika ofisi za kata. Gari lililotubeba lilikuwa nyuma ya gari la RPC ambaye baadaye dereva wake aliendesha kwa kasi kwenda mbele kutaka kuzuia msafara wa CHADEMA.

Lakini viongozi wa CHADEMA walikuwa wameshafika katika ofisi yao ya kata na tukashuka kwenda kushuhudia kinachoendelea. Hapo ndipo tulimkuta Naibu Katibu Mkuu wa CHADEMA, Zanzibar, Hamad Yusuph na viongozi wengine wakisaini katika kitabu cha wageni.

Ghafla, RPC akatoa amri ya kuwakamata viongozi wa CHADEMA waliokuwa katika ofisi yao. Baada ya amri hiyo, wanachama wa CHADEMA waliokuwa pale wote walikaa chini wakinyoosha mikono juu.

Balaa linaanza kwa amri ya RPC Kamuhanda
Baada ya RPC kutoa amri hiyo, polisi walioipokea walianza kurusha mabomu ya machozi kuelekea sehemu waliyokaa wanachama wa CHADEMA. Mabomu hayo yalirushwa na kuumiza wengi, wakiwamo waandishi wa habari. Mimi nilipigwa na kitu chenye kishindo, nikajeruhiwa mkono wa kushoto na sehemu ya paja la mguu wa kulia.

Jitihada za polisi kuwatawanya wafuasi wa CHADEMA zilifanikiwa. Baadhi ya watu na viongozi waliwekwa chini ya ulinzi, sisi tukiwa tunaendelea kufanya kazi yetu ya kukusanya taarifa ili kuhabarisha umma juu ya kile kinachoendelea katika eneo hilo.

Wakati hali hiyo ikiendelea, ofisi za kata za CHADEMA hazikuwa na mtu. Askari wakawa wanapiga mabomu kuelekea ndani ya ofisi hiyo tupu.
Tuliendelea kupiga picha tukio hilo. Ghafla askari mmoja akamgeukia mwandishi wa gazeti la Nipashe, Godfrey Mushi, akaanza kumpiga.

Baada ya kuona mwandishi huyo anapigwa, Mwangosi aliwasogelea askari akitaka kujua sababu za kumshambulia mwandishi wakati yupo kazini kama ambavyo askari hao walivyokuwa wakiwajibika.

Swali la Mwangosi likavuta askari wengine. Wakamzunguka na kuanza kumpiga kwa marungu, mateke na ngumi. Wakati hayo yakifanyika, RPC alikuwa pale anashuhudia.

Baada ya kuona kipigo kimekuwa kikali, Mkuu wa Kituo cha Polisi (OCS) cha Mafinga aliingilia kati kutaka kumnusuru Mwangosi.

Wakati Mwangosi akiwa anashambuliwa, mpiga picha wa gazeti la Tanzania Daima, Joseph Senga, naye alikuwa katika wakati mgumu baada ya askari kumdhibiti na kuanza kumpekua mifukoni, huku mwenyewe akijitahidi kujinasua mikononi mwao.

Mbali na mimi na Senga, muda huo hakukuwa na raia yeyote katika eneo lile, isipokuwa Godfrey Mushi wa Nipashe ambaye sina hakika kama alikuwa anafahamu kinachoendelea maana alikuwa amepigwa sana, yuko hoi.

Baada ya kuona kipigo kinazidi kwa Mwangosi huku Senga akiendelea kupiga picha, uzalendo ulinishinda, nikaamua kumfuata Kamanda wa Polisi mkoani humo aliyekuwa mita zisizozidi kumi ndani ya gari lake, akishuhudia tukio lile. Nikamuomba asaidie kumnusuru Mwangosi na kipigo kile.
 RPC alishusha kioo cha gari lake, akaniangalia, kisha akafunga kioo, huku dereva wake akawa anapiga honi. Sikujua maana ya honi hiyo.
Baada ya kuona hakuna msaada wowote kutoka kwa RPC, nilisogea karibu kwa ajili ya kuendelea kupata picha ya tukio, ili umma ujue juu ya madhila yanayowapata waandishi wa habari mikononi mwa polisi.

Wakati nikiwa naendelea kuchukua picha, nilimwona askari mmoja akinyoosha mkono juu na mwingine aliyevaa kiraia akiwa ameshika bastola yake kuelekeza juu, huku wengine wakiwa wanaendelea kumpiga Mwangosi aliyekuwa anajitahidi kuinuka kwa kumshika mmoja wa askari wale.
Katika harakati za Mwangosi kujinasua, nilimshuhudia mmoja wa wale askari akiwa kama anainama akaelekeza mtutu wa bunduki usawa wa tumbo la Mwangosi aliyekuwa katika hali ya kutaka kusimama huku akipiga kelele “msiniuee, msiniuee…”

Mara nikasikia mlipuko mkubwa pale pale walipo; baadhi ya nyama zikarushwa na kutapakaa, nyingine zikanirukia mimi na kuchafua fulana yangu.

Kumbe walikuwa wamemlipua Mwangosi! Nikapiga picha ya mwili uliosambaratika na kukatika vipande vipande. Nikaona askari wale wanambeba askari ambaye naye alijeruhiwa na mlipuko uliomuua Mwangosi. Nikakimbia kujinusuru na askari wale.

Sikuona tena usalama wangu mbele ya polisi wake. Sikumwamini tena RPC kama angeweza kulinda maisha yangu. Nikatimua mbio kuelekea nisipopajua.
Nikiwa nakimbia nilichomoa kadi ya kamera kutoka katika kamera yangu ili nisipokonywe. Hapo ndipo nilipokutana na mwandishi mwingine, Francis Godwin, nikamwambia asielekee nilikokuwa natoka mimi – ambako ndiko alikuwa anataka kwenda - kwa kuwa Mwangosi ameshauawa na polisi!

Wakati naachana na Godwin, nilichukua simu yangu na kumpigia Mwenyekiti wa Jukwaa la Wahariri, Absalom Kibanda, ambaye ndiye Mhariri Mtendaji wa gazeti hili kwa ajili ya kumpa taarifa. Bahati mbaya simu yake haikupokelewa.
Nikamfuata Makene (Tumaini, afisa habari wa CHADEMA) aliyekuwa amejikinga katika gogo, alikokuwa pamoja na Oliver Motto, nikawaambia eneo hili halitufai watatuua. Ndipo nikampigia simu Bakari Kimwanga, mwandishi wa gazeti la Mtanzania, nikamfahamisha kuwa Mwangosi ameuawa na polisi. Tukakimbilia porini kujificha, kila mtu akiwa analia kivyake.

Baada ya kukaa porini kwa muda, tuliamua kubadilisha nguo zetu ili tusitambulike kirahisi. Tukatoka mafichoni kuangalia hali ya usalama. Tukaanza kuwatafuta wenzetu ambao tulipoteana nao. Baadaye tulikodi teksi kuwafuata wenzetu ambao wakati huo walishakimbia kutoka eneo hilo la hatari.

Tukiwa katika hoteli ya MR mkoani Iringa, mwananchi mmoja alikuja kutueleza kuwa alifanikiwa kukusanya sehemu ya mwili wa marehemu Mwangosi pamoja na mabomu yaliyoachwa katika eneo la tukio na walipoangalia wakaona ni sehemu ya nyama ya utumbo iliyowekwa katika mfuko pamoja na mabomu ya machozi na kuyapanga yale mabomu juu ya meza ya hoteli hiyo na kuyapiga picha huku utumbo wa Mwangosi ukiendelea kuwa katika mfuko uliowekwa.

Hadi sasa sijajua endapo sehemu hiyo ya utumbo ilizikwa usiku ule mkoani Iringa au uliunganishwa na sehemu nyingine ya mwili wake uliotawanywa na bomu hilo kiasi cha kushindwa kujua kama ni mwili wa binadamu au ni ng’ombe aliyechinjwa tayari kwa mauzo.

Hivi ndivyo tulivyompoteza mwandishi mwenzetu, Daudi Mwangosi, akiwa mikononi mwa polisi.

www.freemedia.co.tz

Thursday, September 6, 2012

POLISI ALIYEMUUA MWANGOZI AKAMATWA


POLISI ambaye alifyatua bomu kwa karibu na kusababisha kifo cha Mwandishi wa habari wa Channel Ten,  Daudi Mwangosi, anatarajiwa kufikishwa mahakamani wakati wowote, Fikra Pevu limefahamishwa.

Taarifa za kutoka Iringa zimeeleza kwamba kushitakiwa kwa askari huyo, kunafuatia kukamilika kwa uchunguzi wa awali ambao unathibitisha pasi shaka kwamba bomu alilofyatua ndilo lililosababisha kifo cha mwandishi huyo wa habari.

Imethibitishwa kwamba kilichousambaza mwili wa mwandishi huyo ni bomu maalumu linalorushwa kwa kutumia bunduki kwa nia ya kusambaza watu waliokusanyika kwa nia ya kutenda uhalifu na lilirushwa kwa karibu mno kinyume cha masharti na kanuni za matumizi yake.

Bomu hilo hutakiwa kurushwa kutoka umbali wa mita kati ya60 na 80, wakati askari huyo alilirusha kwa karibu mno na akimlenga mwandishi Mwangosi.

Katika tukio hilo, bomu hilo liliusambaratisha mwili wa Mwangosi na kumjeruhi ofisa mmoja wa polisi ambaye anaelezwa kutaka kumsaidia mwandishi huyo ambaye alikua akipigwa na polisi wenzake.
Marehemu Mwangosi aliuawa Jumapili iliyopita katika kijijini cha Nyololo, wilayani Mufindi, mkoani Iringa katika tukio ambalo Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema) walikuwa wakifungua tawi la chama chao, huku Polisi wakitumia nguvu kubwa kuzuia uzinduzi wa tawi hilo.

Jumuiya Ya Vijana Wa CUF: CUF TUNALAANI MAUAJI YA MWANDISHI WA CHANNEL TEN –...


CUF TUNALAANI MAUAJI YA MWANDISHI WA CHANNEL TEN – IRINGA



Mwenyekiti Wa Cuf Taifa Prof Ibrahim Lipumba-Wa Pili Kushoto akisoma
Tamko,kulia kwake ni Mh Kambaya, kushoto kwake ni Mh Mketo na Mh
Chalamila.
CUF – Chama cha Wananchi tunalaani mauaji ya mwandishi wa Habari wa Channel Ten kituo cha Mkoa wa Iringa yaliyofanywa na jeshi la Polisi, ambaye pia alikuwa ni Mwenyekiti wa Chama cha Waandishi wa Habari mkoani humo (IPC) Daud Mwangosi aliyeuwawa kwa kupigwa na bomu (kama inavyosemekana) katika vurugu za kisiasa baina ya Jeshi la Polisi na Wafuasi wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA) juzi Jumapili, Septemba 2, 2012 katika kijiji cha Nyololo, wilayani Mufindi mkoani Iringa.
Kwa mujibu wa taarifa zinazotatanisha zilizotolewa na Vyombo vya Habari pamoja na kunukuu taarifa za jeshi la Polisi, kuwa Mwandishi huyo aliuwawa kwa mlipuko akiwa mikononi mwa jeshi hilo la Polisi hadi kupelekea hata Askari Polisi waliokuwa karibu yake kujeruhiwa na mwengine kukimbizwa Hospitali.
Taarifa hizo zinazotatanisha zinasema kwamba Mwandishi huyo alikimbilia kwa jeshi la Polisi kama kujisalimisha hadi kufikia kukumbatiana na OCS aliyekuwepo katika eneo hilo la tukio hili ni kwa mujibu wa taarifa ya Jeshi la Polisi, lakini wakati huohuo vyombo hivyo hivyo vya Habari  vinaripoti kuwa Marehemu alikwenda kumtetea mwandishi mwenzake wa vyombo vya IPP Media na Polisi huyo OCS alikuwa akimuhami marehemu asiendelee kupata kipigo kutoka kwa askari wenzake kwani alikuwa akimfahamu, ndipo hapo alipopigwa na mlipuko huo na kutawanya matumbo yake nje.
Tukio kama hili la mauaji  kwa raia katika vurugu za kisiasa baina ya wafuasi wa CHADEMA na Jeshi la Polisi si la kwanza, ukiacha lile lililotokea siku za nyuma kule Arusha lililopelekea watu watatu kuuawa, tukio jengine la kusikitisha ni lile lililotokea Agosti 27, Jumatatu ya wiki iliyopita mjini Morogoro ambapo mtu mmoja alietambulika kwa jina la Ali Nzona (Muuza magazeti) alieuwawa katika vurugu kama hizo, ambapo taarifa zake zinautata wakati ambapo CHADEMA wakidai ameuwawa kwa risasi, taarifa ya Jeshi la Polisi inasema ameuwawa kwa kupigwa na kitu kizito kichwani.
Inasemekana kuwa chanzo cha vurugu zote hizi za Morogoro na Iringa, ni kwa sababu Chama cha Demokrasia na Maendeleo kimekaidi amri ya Jeshi la Polisi kutokukusanyika ama kufanya maandamano katika kipindi hiki cha zoezi la uandikishaji sensa likiendelea hadi hapo litakapomalizika ambapo awali lilipangwa limemalizike Septemba 1, na baadae kuongezwa siku hadi Septemba 8, awali katika makubalino ya CHADEMA na Jeshi la Polisi kabla ya mkutano huo ni kwamba walitakiwa waendelee na mikutano yao.
Kwa mtazamo huu CUF – Chama cha Wananchi tunaona wanaopaswa kubeba lawama hili ni jeshi la Polisi na wala si CHADEMA, kwani kama tulivyoeleza awali ilitosha kuheshimu makubaliano yaliyokuwa yamefanyika baina yao, hata kama kulitokea vurugu haikuhitajika kutumika nguvu kubwa kiasi hiki.
CUF pamoja na kulaani mauaji hayo yanaendelea kutokea lakini pia tunasikitishwa na kupotea kwa nguvu kazi ya Taifa kwa sababu zinazoweza kuepukika, ili hali kuna uwezekano mkubwa kama busara zingetumika kwa pande zote zinazohusika mauaji kama haya yasingetokea, kwani tunaamini katika vurugu kama hizo zilizotokea hakuna zoezi lolote la sensa lililoendelea kufanyika katika maeneo hayo husika kwa wakati huo.
Kama hivyo ndivyo ilivyo hakukuwa na ulazima wowote wakuzuia watu kukusanyika au kuandamana, kwani wanaokusanyika na kuandamana sio wote, bado kuna watu watakao bakia katika makazi yao ambao wangetosha kutoa taarifa za ndugu na jamaa zao ambao hawapo au hata kuhesabiwa kwa siku zingine kwani zoezi bado linaendelea, na waandikishaji sensa wangeweza kuendelea na majukumu yao bila hofu wala vitisho juu usalama wa maisha yao kutokana na vurugu, kama ambavyo ilivyotokea.
CUF – Kwa kipindi kirefu tumekuwa tukilililalamikia jeshi la Polisi kuwa liache kufanya kazi kwa ukada bali lizingatie maadili yake ya kazi ambayo ni kulinda usalama wa raia na mali zake,
matukio kama haya ya jeshi la Polisi yalianza ndani ya chama chetu, ambapo itakumbukwa mauaji ya kimbari yaliyofanywa na jeshi hilo Januari 26 na 27 mwaka 2001 wakati tulipokuwa tukidai Katiba Mpya ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Daftari la Kudumu la Wapiga Kura, Tume Huru ya Uchaguzi na kurudiwa kwa Uchaguzi Mkuu wa Zanzibar wa mwaka 2000.
CUF Tunamuomba Rais Jakaya Mrisho Kikwete kuunda Tume Huru itakayoshirikisha Watetezi wa Haki za Binadamu, Madaktari, Wakuu Jeshi la Polisi na Upelelezi na Wajumbe wengine kutoka vyama vya siasa ili kuchunguza mauaji haya yenye taarifa za kutatanisha, ili kuupata ukweli utakaofanyiwa kazi ya kukomesha mauaji kama haya yasiendelee kutokea, ambayo tunahisi yataendelea kutokea kama hatua madhubuti hazikuchukuliwa.
Prof. Ibrahim H. Lipumba
MWENYEKITI

Wednesday, August 15, 2012

IJUE KATIBA: INASEMA NINI KUHUSU KULINDA TAIFA?

Kwa taarifa yako tu,  Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ya mwaka 1977 ibara ya 18 (3) inasema kwamba:-

"Mtu yeyote hatakuwa na mamlaka ya kusaini Mkataba wa KUKUBALI KUSHINDWA VITA NA KULITOA TAIFA KWA MSHINDI, WALA KURIDHIA KUTAMBUA KITENDO CHA UVAMIZI AU MGAWANYIKO WA JAMHURI YA MUUNGANO AU SEHEMU YOYOTE YA ARDHI YA ENEO LA TAIFA NA BILA KUATHIRI KATIBA HII NA SHERIA ZILIZOWEKWA, hakuna mtu atakayekuwa na haki ya kuwazuia raia wa Jamhuri ya muungano kupigana vita dhidi ya adui yeyote anayeishambulia nchi"

Kwa mantiki hiyo, Kama inabidi kupambana na Malawi basi itakuwa ni mapambano mpaka tone la mwisho,

Kwa kuwa Eneo la Ziwa Nyasa kwa upande wa Tanzania linatambuliwa na Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kama sehemu ya Jamhuri ya Muungano, hivyo basi, kuridhia Wamalawi kuingia nchini kwa namna yoyote ile ni kuvunja katiba ya nchi, 

Kujaribu kuigawanya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa namna yoyote ni Kuvunja katiba ya nchi.

Halafu mwisho, inapofikia hatua Rais anatangaza Vita na adui yoyote anayeishambulia nchi, HURUHUSIWI KUPIGA KAMPENI ZA KUZUIA, AU KUWAZUIA raia wa taifa hili kupigana vita ni Uhaini....unastahili kunyongwa....

I love my Country Tanzania
MUNGU IBARIKI TANZANIA

Sunday, August 5, 2012

"MPANDA NDO HOMIE" IN SUPPORT OF KATAVI YOUTHS

For the first time in the history of Mpanda district and the New Katavi Region, the youths who used to be friends on social networks have decided to make a step from just chatting to serving the society.

This has happened when youths from different kinds of social and educational status decided to put their efforts together and conduct an academic colloquium on 27th June, 2012 that comprised about 400 students from ten secondary schools of Mpanda Urban who came together at The St. Mary's social Hall and discuss several issues concerning their academic success as well social development.

The colloquium aimed at inspiring, motivating and encouraging youngsters in secondary schools to put more efforts in achieving their dreams through academic progress. Several topics were discussed among the students. Topics like; relationships in schools led by Miss Shamila Shaban, Academic performances and progress led by Martin Nyambala, Joseph Kulemba and Frank Banka, Reproductive Health to students led by Miss Felister Mbogo and Gamaliel Raiton, Police Jamii led by the representative from Police force Mr. Ngonyani with the OCS of Mpanda. as well the knowledge about internal tourism led by Mr. Japhari Mkelemi and Idd Fumbo

Frankly speaking, all these presentation were hot and successful as students grasped many important ideas and ways to make their success in life and academics  and that never giving up  and behaving well are the key milestones to their success.

It is now the time for other groups, people and organizations who are committed to conduct different projects and programs for the aim of serving the local people in Katavi so that they play part in then development of their society.

We would like to send our gratitude to all those who made this colloquium to be successful and outstanding, we appreciate all their contributions whether financial or kind contributions, all what was done could not be successful if there were no help from people like these. They are blessed for serving their society.


Friday, August 3, 2012

MALAWI YAITUNISHIA MISULI TANZANIA



  • Yakimbilia mkataba wa Berlin wa kuligawa bara

  • Tanzania yataka suluhisho

  • Msumbiji nao wataka kipande cha ziwa

 
 
Malawi imekataa kuitikia wito wa Tanzania kutaka isimamishe shughuliza kutafuta mafuta na gesi ziwa Malawi, wakati suluhu ya mvutano wa mpaka ikisubiriwa
 
Mvutano wa maneno umezuka kati ya nchi hizo mbili baada ya Malawi kuipa leseni Kampuni ya Uingereza kufanya utafiti katika eneo hilo.
Taarifa zinazohusiana
 
Maafisa nchini Tanzania wanasema mvutano huo uliodumu kwa miaka 50 sasa unaweza kuwa mkubwa iwapo ugunduzi wa mafuta na gesi utatokea kwenye ziwa hilo linalojulikana kama Ziwa Nyasa nchini Tanzania.

Tanzania inasema inaendelea kufanya mazungumzo na Malawi na iko Tayari kulipeleka suala hilo kwenye vyombo vya upatanishi.

"Hili ni suala nyeti sana na tungependa litatuliwe kwa maelewano, tutaendelea na mazungumzo," Waziri wa Mambo ya Nje wa Tanzania alisema.

Membe wiki iliyopita alviambia vyombo vya habari nchini humo kuwa "shughuli za uchimbaji katika eneo la kaskazini mashariki mwa ziwa hazina budi kusitishwa kupisha mazungumzo kutatua mzozo huo yafanyike."

Malawi, koloni la zamani la Uingereza, kwa upande wake iliapa kuendelea na chughuli za utafiti wa hewa gesi mkaa (hydrocarbons).

Tanzania,lililotawaliwa na Ujerumani na baadaye Uingereza, inadai kuwa sehemu ya kilometa za mraba 29,600 sawa na maili 11,400 za ziwa, wakati Malawi inarejea makubaliano ya mwaka 1890 yanaonyesha kuwa mpaka kati ya nchi hizo mbili uko kwenye ufukwe upande wa Tanzania.

Msumbiji pia inadai ina sehemu yake katika ziwa hilo la tatu kwa ukubwa barani Afrika.
Mwezi Septemba mwaka jana serikali ya marehemu Bingu wa iliipa leseni kampuni ya Surestream Petroleum, kutafiti mafuta na gesi ziwani.

Mataifa hayo mawili yatafanya mazungumzo juu ya mpaka kaskazini mwa Malawi katika mji wa Mzuzu Agosti 20 mwaka huu.

Monday, July 23, 2012

WAZIRI AJIUZURU

Waziri wa Miundombinu na Usafirishaji wa serikali ya mapinduzi ya Zanzibar Mh. Hamad Masoud Hamad (Mbunge wa CUF) amejiuzuru wadhifa wake kutokana na mfululizo wa matukio ya Meli Kuzama,  katika kipindi chake akiwa waziri zimezama meli tatu, mbili za abiria na moja ya mizigo,

Rais wa  Zanzibar na mwenyekiti wa Serikali ya Mapinduzi ya  Zanzibar tayari amepokea barua ya kujiuzuru waziri huyo na kumteua mbunge mwingine pia wa CUF kushika wadhifa huo..

Hongera Mh. Hamad kwa kuonesha mfano katika suala la uwajibikaji.

Tafisiri